Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Afrika ya Kati amesisitiza juu ya udharura wa kutekelezwa
kivitendo makubaliano ya amani yaliyotiwa saini hivi karibuni.
Andre Nzapayeke amesema kuwa, ana matumaini
makubaliano ya amani yaliyotiwa saini na wawakilishi wa makundi yote katika
Jamhuri ya Afrika ya Kati yataanza kutekelezwa haraka iwezekanavyo.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati
ameashiria baadhi ya malalamiko na upinzani dhidi ya makubaliano hayo likiwemo
suala la upokonyaji silaha na kubainisha kwamba, hapana shaka kuwa daima kuna
watu ambao hufanya njama za kuvuruga makubaliano, lakini la msingi ni kuwa,
makubaliano hayo yametiwa saini na viongozi wa makundi yote yaliyoshiriki
katika mkutano wa Jamhuri ya Congo Brazzaville.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati
ameutaka Umoja wa Mataifa kutoa ushirikiano unaotakiwa likiwemo suala la
kuhitimisha mapigano na machafuko.
Ikumbukwe kuwa, karibu wawakilishi 170 wa upande wa serikali
na wapinzani walikutana tarehe 21 hadi 23 mwezi huu katika mkutano wa
“Maridhiano ya Kitaifa na Mazungumzo ya Kisiasa” katika mji mkuu wa Jamhuri ya
Congo Brazzaville na kufikia makubaliano ya kurejesha amani na utulivu katika
nchi yao.
0 comments:
Post a Comment